Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Dunia yaanza kuukaribisha mwaka mpya, mataifa ya Pasifiki yaongoza

Sherehe za kuukaribisha mwaka mpya tayari zimeanza katika baadhi ya maeneo ya dunia, huku mataifa ya Pasifiki yakiongoza kuingia mwaka 2026 kabla ya sehemu nyingine za dunia.

Muhtasari

Moja kwa moja

Na Ambia Hirsi & Asha Juma

  1. Sherehe za mwaka mpya katika picha

    Mataifa mbalimbali duniani yanaendelea kuukaribisha mwaka mpya huku saa ya usiku wa manane zikitofautiana katika kanda. hivyo kutofautisha pia wakati wa kuupokea mwaka mpya.

    Mataifa ya Pasifiki yalikuwa ya kwanza duniani kuingia mwaka 2026. Mtalii mmoja aliyekuwa huko alituambia aliuadhimisha mwaka mpya “ufukweni pasipo satelaiti, bila dalili za uwepo wa binadamu, katika giza totoro na katikati ya kaa wengi wasiohesabika.”

    Baada ya hapo, New Zealand ilifuata kwa kuukaribisha mwaka mpya kwa sherehe za fataki (fireworks) katika jiji la Auckland. Hizi ni picha za mbaadhi ya maeneo na namna walivyopokea mwaka mpya 2026.

  2. Dunia yasheherekea mwaka mpya kwa nyakati tofauti

    Dunia inasheherekea mwaka mpya wa 2026, sherehe zikianza kwa kutofautiana muda. Sherehe za kuukaribisha mwaka mpya zilianza katika baadhi ya maeneo ya dunia, huku mataifa ya Pasifiki yakiongoza kuingia mwaka 2026 kabla ya sehemu nyingine za dunia. Miji na visiwa kadhaa tayari vimebadilisha kalenda, vimeshaingia mwaka 2026, huku mamilioni ya watu wakishuhudia fataki, sherehe za kitamaduni na mikusanyiko ya kifamilia kuashiria mwanzo wa mwaka mpya.

    Jiji la Sydney nchini Australia lilikuwa miongoni mwa maeneo ya kwanza yenye watu wengi kuukaribisha mwaka mpya kwa onyesho kubwa la fataki lililopamba anga la Bandari ya Sydney.

    Mamia ya maelfu ya watu walikusanyika kushuhudia tukio hilo, ingawa furaha ilichanganyika na huzuni, baada ya tukio la shambulio lililotokea Bondi Beach mapema mwezi huu, lililoacha majonzi kwa wakazi wa jiji hilo.

    Sherehe pia zikafuatwa katika mataifa jirani ya Pasifiki ikiwemo Fiji, Tonga na Samoa, ambapo wakaazi walikusanyika kwa sala, ngoma za kitamaduni na fataki ndogo ndogo. Wakati huohuo, Kisiwa cha Chatham cha New Zealand, kilicho mbali na bara hilo, kiliingia mwaka 2026 dakika 15 tu baada ya Kiritimati, kikifuata ratiba yake maalum ya muda.

    Kwa upande wa kipekee, mfamasia mmoja kutoka Uingereza tayari ameukaribisha mwaka mpya akiwa Samoa, kabla ya kusafiri kwenda American Samoa, eneo ambalo lina saa tofauti, ili kuukaribisha tena mwaka mpya mara ya pilli, kitendo anachokielezea kama “kusafiri kwenye muda”.

    Mataifa mbalimbali yakafuata kama China, Singapore, Ufilipino, Japan na Korea Kusini, ambako kulifanyika hafla za kupigwa kwa kengele katika miji ya Tokyo na Seoul.

    Baada ya hapo, New Zealand ilifuata kwa kuukaribisha mwaka mpya kwa sherehe za fataki (fireworks) katika jiji la Auckland.

    Kadri saa zinavyoendelea kusogea, mataifa mengine duniani yameendelea kuupokea mwaka mpya ikiwemo ya Afrika, Ulaya na hatimaye Amerika yanayopokea mwaka mpya kwa kuchelewa kidogo

  3. Wezi wavunja benki ya Ujerumani na kutoroka na mamilioni

    Wezi walitumia kipindi cha Krismasi tulivu kuvunja benki ya Ujerumani na kutoroka na pesa zenye thamani ya euro milioni 10 na vitu vya thamani kutoka kwenye masanduku ya amana ya wateja, polisi walisema Jumanne.

    Polisi walisema katika taarifa kwamba wahalifu walitoboa ukuta mzito wa zege katika tawi la benki ya Sparkasse katika mji wa magharibi wa Gelsenkirchen na kisha kuvunja masanduku elfu kadhaa ya amana na kuiba kiasi kinachokadiriwa kuwa mamilioni ya euro.

    Maduka na benki nyingi hufunga nchini Ujerumani wakati wa Krismasi kuanzia jioni ya Desemba 24, na polisi waligundua shimo hilo baada ya kengele ya moto kulia mapema Jumatatu, Desemba 29.

    Wateja wengi wenye hasira walikusanyika mbele ya benki siku ya Jumanne huku wakipaza sauti "Turuhusu tuingie!".

  4. Putin aamuru upanuzi wa eneo la salama la Ukraine mwaka 2026 - Jenerali mkuu wa Urusi

    Jenerali mkuu wa Urusi amesema vikosi vyake vilikuwa vikisonga mbele kaskazini mashariki mwa Ukraine na Rais Vladimir Putin ameamuru upanuzi wa eneo ambalo Moscow inaita ‘eneo salama’ mwaka 2026, mashirika ya habari ya Urusi yalisema Jumatano.

    Mkuu wa Wafanyakazi Valery Gerasimov alisema Putin aliamuru upanuzi wa eneo salama mnamo mwaka 2026 katika maeneo ya Sumy na Kharkiv ya Ukraine karibu na mpaka wa Urusi, RIA ilisema, akiongeza kuwa alikagua kikundi cha wanajeshi wa "Kaskazini".

    Matamshi ya Gerasimov yanafuatia ahadi ya Urusi ya kulipiza kisasi kwa kile ilichodai, bila ushahidi, ilikuwa jaribio la kushambulia makazi ya Putin, madai ambayo Kyiv ilikanusha, ikisema yalilenga kuvuruga mazungumzo ya amani huku vita vikikaribia mwaka wake wa nne.

    Hakukuwa na majibu ya haraka kutoka Ukraine kuhusu ripoti ya Gerasimov.

    Soma zaidi:

  5. Kiongozi wa mapinduzi ya Guinea ashinda uchaguzi wa rais, matokeo yanaonyesha

    Kiongozi wa mapinduzi ya Guinea Mamady Doumbouya amechaguliwa kuwa rais, kulingana na matokeo ya muda yaliyotangazwa Jumanne, na kukamilisha kurejea kwa utawala wa kiraia katika taifa hilo la Afrika Magharibi lenye utajiri wa boksiti na madini ya chuma.

    Kamanda huyo wa zamani wa vikosi maalum, anayedhaniwa kuwa katika umri wake wa mapema wa miaka 40, alichukua madaraka mwaka wa 2021, na kumwangusha Rais Alpha Conde, ambaye alikuwa madarakani tangu 2010. Ilikuwa moja kati ya mfululizo wa mapinduzi tisa ambayo yamebadilisha siasa katika Afrika Magharibi na Kati tangu 2020.

    Matokeo ya awali yaliyotangazwa Jumanne yalionyesha Doumbouya akishinda kwa asilimia 86.72 ya kura za Desemba 28, wingi wa kura unaomruhusu kuepuka duru ya pili ya uchaguzi.

    Mahakama ya Juu Zaidi ina siku nane za kuthibitisha matokeo iwapo kutatokea pingamizi lolote.

    Ushindi wa Doumbouya, unaompa muhula wa miaka saba, ulitarajiwa sana. Conde na Cellou Dalein Diallo, kiongozi wa upinzani wa muda mrefu nchini Guinea, wako uhamishoni, jambo lililomfanya Doumbouya kukabiliana na wapinzani wanane.

    Soma pia:

  6. Mwanaharakati maarufu wa haki za binadamu na mkosoaji wa serikali akamatwa Uganda

    Polisi nchini Uganda imesema imemkamata mwanaharakati maarufu wa haki za binadamu Sarah Bireete, mkuu wa shirika la haki za binadamu na mtoa maoni wa mara kwa mara dhidi ya serikali kwenye televisheni na redio za eneo hilo.

    Polisi ilithibitisha hilo katika chapisho kwenye jukwaa la mitandao ya kijamii X siku ya Jumanne.

    "Yuko chini ya ulinzi wa polisi. Atafikishwa mahakamani kwa wakati unaofaa," chapisho hilo lilisema, bila kutaja ni lini au mashtaka gani anakabiliwa nayo.

    Bireete, mwanasheria na mkurugenzi mtendaji wa Kituo cha Utawala wa Katiba (CCG), amekuwa akikosoa hatua mbalimbali za serikali ikiwemo kile ambacho upinzani unasema ni kuwaweka kizuizini kinyume cha sheria na kuwatesa wafuasi wake.

    CCG haikuweza kupatikana mara moja kutoa maoni.

    Uchaguzi wa Januari unajumuisha Rais aliye madarakani Yoweri Museveni, 81, ambaye amekuwa madarakani tangu 1986, dhidi yamwanamuziki aliyegeuka kuwa mwanasiasa Bobi Wine.

    Wine, mwenye umri wa miaka 43, na chama chake cha National Unity Platform anasema mamia ya wanachama wao wamekamatwa mwaka huu ikiwa ni pamoja na wakati wa kampeni katika hatua iliyokusudiwa kuwatisha wafuasi wake na kudhoofisha ari ya chama.

    Soma zaidi:

  7. Ukraine yasema watu wajeruhiwa katika shambulizi la Urusi

    Urusi imefanya shambulizi usiku kucha la ndege zisizo na rubani katika eneo la Odesa nchini Ukraine, na kuharibu majengo ya makazi na miundombinu na kuwajeruhi watu wanne, wakiwemo watoto watatu, mamlaka za kikanda zilisema Jumatano.

    Odesa, yenye bandari kubwa katika Bahari Nyeusi, imekuwa ikilengwa mara kwa mara na makombora na ndege zisizo na rubani za Urusi wakati wa karibu miaka minne ya vita, huku mashambulizi yakiathiri mara kwa mara miundombinu ya nishati, usafiri na bandari pamoja na maeneo ya makazi.

    "Droni zisizo na rubani zilishambulia miundombinu ya makazi, vifaa na nishati katika eneo letu," Oleh Kiper, gavana wa eneo la Odesa, alisema kwenye programu ya ujumbe ya Telegram.

    Katika jiji la Odesa, ambalo ni kitovu cha utawala cha eneo pana la Odesa, watu wanne walijeruhiwa, ikiwa ni pamoja na mtoto mchanga wa miezi saba, watoto wengine wawili, na mwanamume wa miaka 42, Serhiy Lisak, mkuu wa utawala wa kijeshi wa Odesa, alisema kwenye Telegram.

    Alisema kwamba vifusi vya ndege zisizo na rubani viliharibu madirisha ya majengo kadhaa marefu ya ghorofa.

    Lisak alichapisha picha zinazoonyesha moshi ukitoka kwenye jengo la ghorofa usiku, huku miali ya moto ikionekana kwenye madirisha kadhaa na kile kinachoonekana kama ndege ya maji ya zimamoto iliyolenga sehemu ya mbele ya jengo.

    Soma zaidi:

  8. Taiwan yaendelea kuwa katika tahadhari huku meli za China zikiondoka taratibu

    Taiwan imesalia katika tahadhari kubwa Jumatano baada ya China kufanya mazoezi makubwa ya kijeshi kuzunguka kisiwa hicho siku iliyopita, na kuendeleza kituo chake cha dharura cha baharini huku kikifuatilia jeshi la majini la China, walinzi wa pwani walisema.

    Mazoezi hayo yaliyopewa jina la "Justice Mission 2025" yalishuhudia China ikirusha makombora kadhaa kuelekea Taiwan na kupeleka idadi kubwa ya meli za kivita na ndege karibu na kisiwa hicho, katika onyesho lililosababisha wasiwasi kutoka kwa washirika wa Magharibi.

    Taiwana ilishutumu mazoezi hayo kama tishio kwa usalama wa kikanda na uchochezi wa wazi.

    Meli za China zilikuwa zikiondoka kutoka Taiwan, lakini Beijing ilikuwa bado haijatangaza rasmi mwisho wa mazoezi hayo, kulingana na Kuan Bi-ling, mkuu wa Baraza la Masuala ya Bahari la Taiwan.

    "Hali ya baharini imetulia, huku meli na vyombo vingine vikiondoka taratibu. Huku China ikiwa haijatangaza kukamilika kwa mazoezi ya kijeshi, kituo cha dharura cha China kinaendelea na shughuli zake," alisema katika chapisho kwenye Facebook Jumanne jioni.

    Afisa wa walinzi wa pwani wa Taiwan aliambia Reuters kwamba meli zote 11 za walinzi wa pwani wa China zilikuwa zimeondoka majini karibu na Taiwan na zinaendelea kuondoka. Afisa wa usalama wa Taiwan alisema vituo vya dharura vya jeshi na walinzi wa pwani vinaendelea kufanya kazi.

    Soma zaidi:

  9. Thailand yawaachilia huru wanajeshi 18 wa Cambodia

    Thailand imewaachilia huru wanajeshi 18 wa Cambodia waliokamatwa mwezi Julai wakati wa mapigano makali ya mpakani kama sehemu ya makubaliano ya kusitisha mapigano ambayo nchi hizo mbili zilikubaliana Jumamosi.

    Makabidhiano ya wafungwa yalicheleweshwa kwa siku moja kutokana na wasiwasi wa Thailand kuhusu madai ya ukiukwaji wa makubaliano ya kusitisha mapigano, lakini yalifanyika baada ya shinikizo la kidiplomasia la China kuendelea kuhakikisha makubaliano hayo yanadumu.

    Mvutano mkali katika mpaka wa Thailand na Cambodia ulilipuka mapema mwezi huu na kuendelea kwa wiki kadhaa, na kulazimisha karibu watu milioni moja kukimbia majumbani mwao.

    Mkataba wa Jumamosi ulishuhudia pande zote mbili zikikubaliana kusitisha mapigano kwa sasa, kupiga marufuku vikosi vya kijeshi na kuruhusu raia wanaoishi katika maeneo ya mpakani kurudi haraka iwezekanavyo.

    Pia unaweza kusoma:

  10. DR Congo kushirikiana na Uingereza kuwarejesha nyumbani wahamiaji haramu

    Mamlaka katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo inasema kuwa serikali inashirikiana na Uingereza kutafuta suluhu la pamoja kuhusu kurejeshwa nyumbani kwa raia wa Congo wanaoishi nchini humo kinyume cha sheria.

    Taarifa kutoka kwa wizara ya habari ilisema serikali imefahamishwa rasmi, kupitia njia za kidiplomasia, juu ya hatua zinazozingatiwa na serikali ya Uingereza kuhusu kuanzishwa kwa vikwzo vya viza vinavyolenga wamiliki wa hati maalum za kusafiria za Congo.

    Kwa mujibu wa taarifa hiyo maafisa wa nchi zote mbili wanaendelea na taratibu za awali zautambuzi wa watu wanaohusika kwani mpango wa kuwafukuza hauwezi kuanzishwa kukiwa na mashaka yoyote kuhusu utambulisho na kwamba mchakato huo ni sharti ufanyike kwa kuzingatia kikamilifu haki za binadamu.

    Pia unaweza kusoma:

  11. Mali na Burkina Faso zawawekea vikwazo vya usafiri raia wa Marekani

    Mali na Burkina Faso zinasema zitawazuia raia wa Marekani kuingia katika nchi zao, katika kile wanachoeleza kuwa ni jibu la moja kwa moja kwa uamuzi wa Washington wa kuwazuia raia wao Marekani.

    Mataifa hayo mawili ya Afrika Magharibi yanayoongozwa na kijeshi yalitangaza hatua hiyo Jumanne usiku, yakisema hatua hiyo inaanza mara moja.

    Uamuzi huo unafuatia vikwazo vya usafiri vya Marekani vinavyoathiri mataifa kadhaa barani Afrika na Mashariki ya Kati, kuliidhinishwa na Rais Donald Trump.

    Wizara ya mambo ya nje ya Mali ilisema inatekeleza kanuni ya usawa, na kuongeza kuwa raia wa Marekani sasa watakabiliwa na masharti yale yale ya kuingia nchini Mali yaliyowekwa na Marekani.

    Serikali ya Burkina Faso imesema itaendelea kujitolea kudumisha usawa wa uhuru, na kwamba bado iko wazi kwa ushirikiano na washirika wa kimataifa ambapo maslahi yanalingana.

    Mali na Burkina Faso, pamoja na nchi jirani ya Niger, hivi majuzi zilijiondoa katika jumuiya ya kikanda ya Afrika Magharibi Ecowas na kuunda Muungano wa Mataifa ya Sahel.

    Mataifa hayo yamejitenga na washirika wa Magharibi na kuimarisha uhusiano na Urusi.

    Nchi nyingine za Kiafrika zilizoathiriwa na marufuku iliyopanuliwa ya hivi karibuni ya Marekani, ikiwa ni pamoja na Nigeria na Sierra Leone, zimesema zinapanga kujibu kupitia njia za kidiplomasia.

    Hatua za Marekani zinapaswa kuanza kutumika tarehe 1 Januari 2026.

    Mapema mwaka huu, Chad pia ilichukua hatua ya kulipiza kisasi baada ya kujumuishwa katika awamu ya kwanza ya vikwazo, kusitisha utoaji wa viza kwa raia wa Marekani.

    Rais Mahamat Idriss Déby Itno alisema hatua hiyo inahusu utu wa taifa, akiongeza kuwa Chad inaweza kukosa utajiri au ushawishi, lakini haitakubali kudhulumiwa.

    Pia unaweza kusoma:

  12. Israel yazuia mashirika 37 ya misaada kuhudumu Gaza

    Israel itafutilia mbali leseni za mashirika 37 ya misaada yanayohudumu huko Gaza na Ukingo wa Magharibi unaokaliwa, ikisema wameshindwa kukidhi mahitaji chini ya sheria mpya za usajili.

    Mashirika maarufu ya kimataifa yasiyo ya kiserikali kama vile ActionAid, International Rescue Committee na Shirika la Wakimbizi la Norway ni miongoni mwa yale ambayo leseni zao zitafutwa kuanzia tarehe 1 Januari, na shughuli zao kufungiwa ndani ya siku 60.

    Israel imesema mashirika hayo, miongoni mwa mambo mengine, yameshindwa kupeana taarifa "kamili" za kibinafsi za wafanyakazi wao.

    Hatua hiyo imekosolewa vikali na mawaziri wa mambo ya nje kutoka nchi 10 ikiwemo Uingereza, ambao walisema sheria hizo mpya ni "vizuizi" na "hazikubaliki".

    Katika taarifa ya pamoja, mawaziri wa mambo ya nje wa Uingereza, Ufaransa, Kanada, Denmark, Finland, Iceland, Japan, Norway, Sweden na Uswisi walisema kufungwa kwa lazima kwa shughuli za mashirika ya kutoa misaada ya kiutu "kutakuwa na athari kubwa katika upatikanaji wa huduma muhimu ikiwa ni pamoja na huduma za afya".

    Waliongeza kuwa hali ya kibinadamu mjini Gaza ni "janga" na kutoa wito kwa serikali ya Israel kuhakikisha mshirika yasiokuwa ya kiserikali yanaweza kufanya kazi "bila kuhangaishwa".

    Wizara ya Masuala ya Kigeni ya Israel, ambayo inasimamia maombi ya usajili, ilisema hatua hizo mpya hazitaathiri mtiririko wa misaada ya kibinadamu kwa wakazi wa Gaza.

    Soma pia:

  13. UAE kuondoka vikosi vyake Yemen kufuatia shambulizi la Saudia

    Umoja wa Falme za Kiarabu umesema kuwa utaondoa vikosi vyake vilivyosalia nchini Yemen, baada ya Saudi Arabia kuunga mkono matakwa ya baraza la rais la Yemen la kutaka waondoke ndani ya saa 24.

    Tangazo hilo la Imarati lilifuatia shambulio la anga la muungano wa kijeshi unaoongozwa na Saudi Arabia dhidi ya kile ilichokisema kuwa ni shehena ya silaha kwa ajili ya wanajeshi wanaotaka kujitenga wanaoungwa mkono na UAE katika bandari ya kusini ya Mukalla.

    UAE imekanusha shehena hiyo ilikuwa na silaha na ikaelezea "kusikitishwa sana" na tuhuma za Saudia.

    Saudia na UAE zimekuwa washirika katika vita dhidi ya vuguvugu la Wahouthi la Yemen linaloungwa mkono na Iran katika kipindi cha muongo mmoja uliopita, lakini mapigano kati ya makundi hasimu yanayounga mkono yamezidisha mpasuko kati yao.

    Saudi Arabia pia ilishutumu UAE kwa "kuwashinikiza" wanaotaka kujitenga kushambulia vikosi vya serikali inayoungwa mkono na Saudia katika majimbo mawili ya mashariki, na kuonya kuwa itachukua hatua kukabiliana na vitendo kama hivyo "hatari sana".

    Siku ya Jumanne mchana, wizara ya ulinzi ya UAE ilitoa taarifa ikitangaza "kusitishwa kwa operesheni ya kupambana na ugaidi nchini Yemen kwa hiari yake", miaka sita baada ya vikosi vya kijeshi vya UAE "kuhitimisha" uwepo wao.

  14. Mwanamume aliyeonekana akipiga risasi kwenye tamasha la AfroFuture akamatwa Ghana

    Polisi nchini Ghana wamemkamata mwanamume aliyenaswa kwenye video ya mtandaoni akifyatua bunduki wakati wa tamasha la muziki mjini Accra.

    Mshukiwa huyo, aliyetambulika kama Abubakari Sadick, maarufu kama "Cyborg", alitoa bunduki hiyo wakati wa mkutano na mwanamuziki wa Nigeria Asake, kinyume na Sheria ya Silaha za Moto na Sheria ya Utaratibu wa Umma.

    Alikamatwa na Timu ya Uchunguzi wa Mtandao (Cyber ​​Vetting Team) katika Makao Makuu ya CID baada ya watumiaji wa mitandao ya kijamii kutaka akamatwe kwa kutoa silaha hiyo kiholela kwenye hafla ya hadhara.

    "Kikosi cha Uchunguzi wa Mtandaoni katika Makao Makuu ya Idara ya Upelelezi wa Jinai (CID) kimemkamata mshukiwa aliyeonekana kwenye video akionyesha bunduki ya hali ya juu kwenye tamasha la AfroFuture lililofanyika katika Uwanja wa El-Wak, Accra, tarehe 28 Desemba 2025."

    "Kwa sasa mshukiwa yuko chini ya ulinzi wa polisi, akisaidia katika uchunguzi, na atafikishwa mahakama kujibu haki," Inspekta Mkuu Brigitte Babanawo alisema katika taarifa.

    Silaha iliyoonekana mtandaoni, iliyotambuliwa kama bunduki aina ya Derya MK-12, imechukuliwa kutoka kwa mshukiwa kama ushahidi.

    Polisi nchini Ghana pia wametoa tahadhari kwa umma juu ya matumizi mabaya ya silaha, wakisisitiza kuwa kumiliki silaha iliyosajiliwa hakumpatii mmiliki uhuru wa kuitumia kiholela.

  15. Marekani yazuia pesa za malezi ya watoto Minnesota kufuatia madai ya ulaghai

    Utawala wa Trump umesema umezuia malipo ya malezi ya watoto kwa jimbo la Minnesota baada ya mshawishi wa YouTube wa kihafidhina kudai kuwa vituo kadhaa vinavyoendeshwa na wahamiaji wa Kisomali vinachukua pesa za umma bila kutoa matunzo.

    Katika chapisho kwenye X siku ya Jumanne, afisa wa juu wa Idara ya Afya na Huduma za Kibinadamu (HHS) alinukuu video hiyo iliyosambaa sana mitandaoni, na kusema shirika hilo litalenga "udanganyifu wa wazi ambao unaonekana kukithiri jimbo la Minnesota".

    Maafisa wa serikali wamerudi nyuma dhidi ya madai ya ulaghai kwenye video hiyo.

    Utekelezaji wa sheria za uhamiaji hivi karibuni umeongezeka katika jimbo hilo, ambalo lina idadi kubwa ya wahamiaji wa Kisomali nchini Marekani, baada ya Rais Donald Trump kusema hataki waingie nchini humo. "Tumezuia malipo yote ya malezi ya watoto kwa jimbo la Minnesota," Naibu Katibu wa HHS Jim O'Neill alitangaza katika ujumbe katika mtandao wa X siku ya Jumanne.

    Alisema uamuzi huu unafuatia "madai mazito kwamba jimbo la Minnesota limeelekeza mamilioni ya dola za walipa kodi kwa vituo ghushi vya kulelea watoto kote Minnesota katika muongo mmoja uliopita".

    Idara hiyo ilisema itasitisha malipo ya kila mwaka ya $185m (£137m) kwa jimbo hilo, ikisubiri ukaguzi kamili wa vituo husika.

    Video ya Nick Shirley, ambayo imepokea mamilioni ya watu kwenye mitandao mbalimbali ya kijamii tangu kuchapishwa mwishoni mwa juma, ilishutumu takriban vituo kumi na mbili kwa kutotoa huduma yoyote au kuwa na watoto wowote wakati Bw Shirley alipovitembelea.

    Pia unaweza kusoma:

  16. Hujambo na karibu

    Nakukaribisha katika taarifa zetu za moja kwa moja, leo Jumatano tarehe 31 Disemba 2025