Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.
Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data
George HW Bush: Mbwa wa rais wa zamani Sully agusa wengi kwa heshima zake za mwisho
Mbwa aliyekuwa amepewa kazi ya kuwa msaidizi wa rais wa zamani wa Marekani George HW Bush amepigwa picha akionekana kuomboleza karibu na jeneza la kiongozi huyo.
Bw Bush, aliyehudumu kama rais wa 41 wa Marekani kati ya mwaka 1989 na 1993 alifariki dunia Ijumaa usiku akiwa na miaka 94.
Sully, mbwa wa jamii ya golden labrador, alisafiri pamoja na mwili wa marehemu kwenye ndege kutoka Texas kwenda Washington DC siku ya Jumatatu.
Jeneza lenye mwili wake lilisafirishwa kwa ndege kutoka Texas kwenda DC kwa ndege ya Air Force One - ambayo kwa muda ilipewa jina Special Air Mission 41, kwa heshima ya rais huyo.
Mwili huo ulirejeshwa Texas Jumatano.
Mbwa huyo wa jina Sully alisindikiza jeneza hilo muda wote.
Picha ya kwanza kabisa ya Sully akitoa heshima zake ilipakiwa mtandaoni na msemaji wa Bw Bush Jim McGrath, pamoja na ujumbe: "Mission complete."
Watu katika mitandao ya kijamii wamekuwa wakimshukuru Sully kwa huduma zake, na kwa kawaida kuzungumzia uaminifu wa mbwa kwa wamiliki wao.
Sully amepewa jina la rubani wa ndege za abiria Chesley "Sully" Sullenberger, ambaye alifanikiwa kuielekeza ndege ya kubeba abiria kutua kwa dharura kwenye Mto Hudson mwaka 2009, na kuwaokoa abiria wote 155 na wahudumu waliokuwa kwenye ndege hiyo.
Mbwa huyo mwenye miaka miwili alikabidhiwa jukumu la kuwa mbwa msaidizi wa Bush aliyekuwa akitumia kiti cha magurudumu mapema mwaka huu.
Sully ni mbwa aliyepokea mafunzo sana, na anaweza kutekeleza maagizo mengi, ikiwemo kufungua milango na kuchukua vitu vinavyohitajika na mmiliki wake, mfano simu inapoita.
Sasa atahudumu kama mbwa msaidizi kwa wanajeshi waliojeruhiwa vitani.
Sully ana ukurasa wake kwenye Instagram, na hapa anaoneshwa akimsaidia Bw Bush kupiga kura wakati wa uchaguzi wa katikati ya muhula mwezi jana.
Sio marais wote wa Marekani wanaowapenda mbwa hata hivyo.
John F Kennedy hakuwapenda kamwe, na Donald Trump hana mbwa. Lakini Barack Obama anawapenda mbwa sana.
Rais Bush amekuwa akipokea matibabu ya ugonjwa wa Parkinson na alilazwa hospitalini akiwa na tatizo la maambukizi kwenye damu mwezi Aprili.
Alifariki akiwa na miaka 94 mjini Houston, Texas.
Atazikwa kwenye maktaba ya rais Texas, karibu na mkewe, Barbara Bush, aliyefariki dunia miezi saba iliyopita.